Kama ilivyo chunvi ya dunia,
ufugaji pia huhitaji upendo, uvumilivu, karama, utu na maombi ya dhati
ambayo yatazaa namna nzuri ya kuipenda kwa dhati ya moyo wako kazi hii
ya ufugaji. Vinginevyo utabakia kuwa mtu wa kujaribu na kuishia
kushindwa kila mara. Kama ilivyo kanuni ya maendeleo yoyote yale,
ufugaji wa kuku pia huhitaji;
Ubunifu,
utundu wa akili, kujaribu bila kukata tamaa, kugundua, kujifunza,
kufanyia kazi mawazo yaa wengine, kusoma vitabu na majarida mbalimbali
yahusuyo kazi yako, kujishughulisha nk. Hata
ukifundishwa darasani huwezi kufundishwa vyote na mwalimu wako, vingine
itakubidi utafute mahali pengine kwa ubunifu mkubwa, ugunduzi na mambo
mengine mengi ili ufanikishe lengo la kupata elimu bora ya kile
unachokitaka. Hii huhusisha akili yako vema katika kujifunza kutoka kwa
watu au vitu vingine nk. Lakini mafanikio zaidi yatapatikana pale utakapokuwa katika utendaji zaidi.
Ikumbukwe
kwamba, kujifunza kwa msisimko tu bila ya kuyaingiza mambo hayo
uliyojifunza katika mazoezi na vitendo vya makusudi maishani mwetu ni
wazi kwamba hayatatusaidia, bali yatabaki vichwani mwetu kama hadithi tu
za alfulelaulela na maisha ya kubahatisha maarufu kama akadabraakadabra.
Hivyo tumuombe sana Mungu wetu ili mafundisho haya yaweze kubadili
maisha yetu kwa uchumi bora na endelevu ili tuweze kupata kipato na
kurudishia Mungu zaka na sadaka badala ya kukaa kulalamika kuwa hatuna
cha mkurudishia muumba wetu Mungu Mtakatifu.
Kuna usemi flani unatumiwa na watu wengi sana. unasema; “kazi ndio msingi wa maendeleo ya mtu yeyote” . Hata
mimi nakubaliana na usemi huu kwani ni kweli kabisa kazi ndio msingi wa
hatua yoyote ya maendeleo ya mtu yeyote chini ya msingi mkuu ambao ni
Mungu. Kinyume chake, asiyefanya kazi (ya kuajiriwa/kujiajiri) basi
atabaki kuwa maskini na mtu wa shida ya kipato, mahusiano mabaya na
wanadamu wenzako, kuwa tegemezi nk. Kwa kuwa tunatamani sana kutoka
katika kongwa hili la umasikini wa kipato na hali mbaya ya maisha,
tunalazimika kufanya jukumu letu kuu la kumuomba sana Mungu ili
atuwezeshe kujua na kufahamu mbinu mbalimbali kisha kujifunza na
kufahamu kwa makini tena kwa njia rahisi mno za kututoa katika hali hii
ya umaskini uliokithiri.
(Kuku 200 x 5,000 = 1,000,000)
Unaweza
ukaniona kama mimi ni kichaa na ninaye ota ndoto za mchana ambazo
hazina mafanikio wala tija maana nadharia hii inaweza isiwaingie vizuri
watu vichwani mwao. Watu wengi wamekuwa wakisema na kushauri hata
kushauriwa hata na wale wasiofaa. Ninaamini wengi wetu hawapendi kuamini
kile wanachoambiwa hadi pale watakapoona kwa macho yao ndipo waamini (akina Tomaso). Sikia nikuambie! kama
huamini haraka kitu chochote hebu usimkatishe tamaa yule aliyekwambia
habari hizo za kukatisha tamaa, badala yake jaribu kupeleleza na
kufuatatilia hatua kwa hatua tena kwa makini maelezo uliyopewa, kisha
yaweke katika utendaji (tenda/fanya) kwa ufanisi kisha subiri matokeo.
Baada ya kupata matokeo sasa unaweza kwenda mbele kidogo
ukauliza/kusoma/kujifunza zaidi ili kuona kama kuna mahali umekosea au
hukuzingatia kanuni na maelekezo uliyopewa. Baada ya kupata maelezo ya
ziada hebu rudia kufanya tena kwa kuboresha kupitia
maelekezo ya awali na hayo mapya uliyopata yote kwa pamoja ili upime
matokeo yake. Hapo sasa utakuwa upo kwenye haki ya kuamini au kutoamini
kwamba jambo hilo ni kweli au siyo kweli na siyo kutaa tu kwa ubishi
usiokuwa na maana yeyote. Kwa kufanya hivi hakika utapiga hatua mbele
katika kuboresha maisha yako ya sasa na ya baadae. Ila ukifanikiwa usije ukamkufuru Mungu aliyekuwezesha.
Hebu anza na kuku Watano (5) tu
Majike wenye Rika/Umri mmoja (au wanaokaribiana). Watunze vizuri kwa
kuwapatia chakula kilicho na mchanganyiko kamili wa viini lishe
vinavyotakiwa katika mwili wa kuku, yaani; wanga, protini, calcium, chumvichumvi, madini joto nk (kama nilivyoeleza hapa chini). Wawekee na Jogoo mmoja mzuri wa kienyeji/kizungu/chotara (kama nilivyoeleza hapa chini juu ya uchaguzi wa majogoo).
Wanapoanza
kutaga watayarishie mahali pazuri/Kiota kizuri cha kutagia na kuatamia
kwa kuwajengea viota ndani ya banda. Hakikisha mahali hapo hapavuji wala
hapapati unyevunyevu wala joto kali sana. Hakikisha mahali hapo pana
usalama wa kutosha (mahali wanyama hatari kama vicheche, pakashume,
nyoka nk hawawezi kufika).
Kuku
wakiendelea kutaga na sasa ukaona wanakaribia kuatamia,Anza kuchagua
aina ya mayai unayotaka kuku wako walalie. Hii inamaanisha kuwa;
ukichagua mayai makubwamakubwa hayo yanakuwa na vifaranga majogoo na mayai madogomadogo mara nyingi huwa ni ya vifaranga majike. Acha kuwawekea mayai ya mviringo kama mpira!
Hakikisha kuku wote wanasubiriana ili walalie/waatamie kwa pamoja.
Weka
mayai 12 hadi 15 kwa kila kiota cha kuku 1 kulingana na umbo la kuku
wako. Kuku anaweza kutaga hadi mayai 30 kwa kila msimu wa kutaga
unapofika. Unaweza kutumia mayai machache kati ya 30 kwa kumuatamishia
kuku wako huku mayai mengine yakisubiri awamu ya pili ya kuatamiwa.Kwa
mfano ukiwawekea kuku wako hao watano,Kuku 5 x Mayai 12 = Mayai 60.
Kwa
kawaida kuku huatamia/hulalia mayai kwa siku 19 hadi 21/24 tu hadi
anapototoa vifaranga. Hakikisha unawawekea kuku walioatamia chakula
chenye viini lishe vya kutosha na maji mengi karibu na viota vyao ili
wakitoka kwenye viota vyao wale chakula mara moja na kunywa maji kisha
warudi haraka kwenye mayai yao. Hii itasaidia kuangua mayai yote 12/15
bila kuharibu yai hata moja. Au hata yakiharikbika basi hayataharibika
mengi kama ukiacha kuwawekea chakula waende kufukuzana na panzi na
vyakula majalalani huko nje na kuchelewa kurudi kwenye mayai yao.
Wakati
ukisubiria siku hizo 21/24 anza kujenga kibanda kidogo ndani ya banda
kubwa ulilojenga awali au jikoni au andaa boksi kubwa na gumu kwaajili
ya kutunzia vifaranga watakaoanguliwa ndani ya siku 21/24 zijazo.
Baada ya kuku hao 5 kuangua vifaranga wako 60 hapo
ndipo kazi kubwa ya kulea vifaranga inapoanza. Elewa kuwa ili upate
mafanikio haraka hakikisha kuwa kazi ya kulea vifaranga inakuwa yako na
siyo ya kuku! Kwanza,Unatakiwa
kuondoa na kuchoma moto/kufukia mabaki yote ya mayai na kuboresha usafi
wa banda lote ili kuepusha magonjwa kama vile kuharisha, viroboto,
papasi nk. Hapo unaweza kuwatoa vifaranga wako wote 60 mmojammoja kadri
wanavyoanguliwa hadi kufikia kifaranga wa mwisho, yaani Yule wa 60 na
kuwaweka katika kibanda kidogo/boksi ulichokijenga na kuwawekea mayai
mengine mama zao (yale 15/18 kati ya 30 uliyoyabakiza) ili waatamie tena
kwa siku 21 hadi 24 zingine. Unapotoa kifaranga kutoka kwa kuku
aliyeatamia humfanya kuku Yule ashindwe kutoka kwenye mayai maana hana
mtoto wa kulea.
Akimaliza
kuangua mayai yote na ukamuwekea mengine ni rahisi kwake kuendelea
kuatamia maana atasubiri kupata vifaranga na ndipo atajikuta amelalia
kwa siku 21 zingine bila wasiwasi. Kwa kufanya hivyo utakuwa tayari
umejipatia vifaranga/kuku zaidi ya 100 ndani ya wiki 7 tu! Sasa Unatakiwa kuwajali sana kuku hawa wanaolalia kwa mara ya pili kwa kuwapa chakula cha kutosha, maji, majani ya makongwe, mchicha, mchunga nk ili
wapate vitamini na madini mengine muhimu kwa afya zao. Fanya hivyo hata
watakapokuwa wametotoa na ukawanyang’anya vifaranga. Hii itawasaidia
ili wasinyonyoke sana manyoya maana kuku wengi hunyonyoka manyoya
wanapoatamia. Kwa kufanya hivi, kuku wako watakaa kwa wiki 2 hadi 3 bila
vifaranga na kisha wataanza kutaga tena na kuatamia kama mwanzo.
Vifaranga wako hakikisha unawatengenezea chumba chao kido ndani ya banda kubwa/jikoni, kisha wawekee chanzo chochote cha joto kama vile; taa ya chemli/jiko la mkaa/vizinga vya moto nk ili wasiathiriwe na baridi hasa wakati wa usiku. Umakini mkubwa sana unatakiwa hapa! Hakikisha
unakuwa makini wakati wa usiku ili kuongeza na kupunguza joto ndani ya
kibanda cha vifaranga maana wakati huu maranyingi joto hupungua na
ubaridi huongezeka na hivyo unaweza kuua vifaranga wako.
Katika
ulezi wa vifaranga kama kuku utawanyang’anya vifaranga vyao utatakiwa
kuwajengea banda dogo (ndani ya banda kubwa/uzio) ili uwawekee chanzo
cha joto kama taa/jiko la mkaa (kama ni sehemu/majira ya baridi). Kama
utatumia jiko la mkaa unatakiwa kuacha kwanza hadi mkaa mweusi uwake
wote ndipo uweke bandani maana mkaa ukitoa moshi unaweza kuathiri
vifaranga vyako. Angalia namna ya kuweka jiko lako la mkaa juu kidogo
ili vifaranga wasiungue. Hakikisha taa yako haitoi moshi sana na
haivujishi mafuta. Pia uwe na akiba ya mafuta ya taa ya kutosha. Usiweke
mafuta mengi kwenye taa maana inaweza kulipuka ikakuletea hasara. Vifaranga wasizidi 50 kwa boksi 1.Hakikisha
umewasha taa/jiko lako ndani ya boksi saa tatu au zaidi kabla ya
kuwaweka vifaranga ili chumba/boksi lipate joto kabla ya vifaranga
kuwasili. Njia hizi zinahitaji uangalifu wa hali ya juu sana kwani
kuhatarisha/kuua vifaranga ni kuhatarisha maendeleo yako. Kama utaamua
kutumia umeme pia ni vizuri zaidi maana inapunguza hatari zaidi.
Kwa hiyoa njia zote tatu unaweza kutumia jedwali lifuatalo ili kuweza kumeneji joto la kibanda cha vifaranga;
UMRI WA KKUKU/VIFARANGA | JOTO NDANI YA BOX/KIBANDA CHA KULELEA VIFARANGA | JOTO NDANI YA CHUMBA/BANDA |
Wiki 1 | 33-35oc | 30-32oc |
Wiki 2 | 30-33oc | 27-29oc |
Wiki 3 | 27-31c | 24-26oc |
Wiki 4 | 24-29oc | 21-23oc |
Wiki 5 | 26-27oc | 22-23oc |
Baada ya wiki ya 4/5 pasua box/watoe kwenye banda la kulelea ili walelewe kwa joto la kawaida la banda/chumba.
Kwa
kawaida joto hupimwa kwa kipimajoto (thermometer), lakini kama huna
kipimo hiki, njia rahisi ni kuwaangalia kulingana na tabia zifuatazo; Kama
vifaranga wamejikusanya sehemu moja basi joto ni kidogo bandani mwao,
au kama wanaenda mbali na chanzo cha joto huku wanatanua mabawa yao na
wakihema harakaharaka basi joto ni kali/limezidi kiwango. Pale watakapo
tawanyika vizuri ndani ya boksi/kibanda cha kulelea huku wanakula na
kunywa maji vizuri basi joto ni la wasta na ndilo linalofaa. Kama unatumia njia ya Boksi, basi unatikiwa kulipanua kulingana na ukuaji na mahitaji ya vifaranga vyako.
Vifaranga
wako wape chakula cha vifaranga cha kutosha, maji safi na salama,
majani mabichi ambayo hufungwa kwa kuning’inizwa kwa kamba,na CHANJO za
minyoo nk ili wapate vitamin, madini na protini itakiwayo na kuzuia
tabia ya kudonoana ili wakue vizuri.
Hakikisha
kuwa chumba chao ni kisafi na hakina unyevunyevu wakati wote.
Unyevunyevu husababisha ugonjwa wa baridi na hufanya vifaranga
wajikunyate na kutetemeka na wanaweza kufa ghafla!
Inashauriwa
kuwa siyo salama kufuga aina nyingine ya ndege kama vile njiwa, bata,
bata mzinga nk kwa kuwachanganya na kuku maana kila aina ya ndege
wanamagonjwa yao. Hivyo kuwachanganya kutakufanya ushindwe namna ya
kuwatibu wanapopatwa na ugonjwa. Pia chawa wa njiwa huleta ugonjwa wa
Ndui hasa kuku wanapoangua vifaranga wao. Hapa ugonjwa unaweza kufyeka
vifaranga wako wote 60/100 kama utafuata ushauri wangu!
Baada
ya wiki 2 hadi 3 baada ya kuwanyang’anya vifaranga kuku wako wataanza
tena kutaga mayai. Wakiatamia wote 5 Kama utaimarisha huduma kwao na kwa
vifaranga/kuku wale 100 tayari utakuwa una kuku 105 au zaidi. Kuku wale
5 wa mwanzo wakiatamia tena kwa siku 21 hadi 48 (kama utafuata mfumo
ule wa mwanzo wa kuaatamishia mara 2) utajipatia vifaranga wengine 100 tena na hivyo kuwa na kuku zaidi ya 200 ndani ya miezi 5/6 tu! Ukiwahudumia
vifaranga wale wa mwanzo 100 vizuri kwa miezi 3 na nusu nao wataanza
kutaga kama mama zao. kwahiyo, Chukulia walalie majike 5 wa mwanzo na
majike 50 waliopatikana baada ya uzao wa kwanza kwa miezi ile 3 ya
mwanzo utakuwa na mitetea 55. Wote wakiatamia na watoe vifaranga 10 kila
mmoja kwa siku zilezile 21 hadi 46, tayari utakuwa na vifaranga 550! Sasa jumlisha na wale 150 waliobakia kati ya kuku 200 na wote wakakua vizuri utapata kuku na vifaranga zaidi ya 700! Jumlisha na 550 watakaototolewa na mama zao wale 5 wa kwanza na wale 50 wa uzao wa 1 na 2 kwa mara ya 2 si tayari utakuwa na kuku zaidi ya 1,200 ndani ya miezi 6 hadi 8 tu? Hivyo utajikuta unao kuku zaidi ya 1,000!
Kati ya kuku 1,000 ukisema utoe kuku 800 wa kuuza na ukiwauza kwa bei ya Tsh. 4,000 kwa kila kuku 1 tayari utakuwa na Jumla ya Tsh. 3,200,000/= ambazo
unaweza kufanya mtaji wa mambo mengine au kuboresha mradi wako zaidi.
Unafikiri hapo hujaanza kufikia lengo la kuku 1 akuletee shilingi
Milioni 1? Ukiendelea hivi inamaana kuku 1 atakuzalishia zaidi ya hapo.
BANDA LA KUKU.
Unatakiwa kuwa na banda bora la kufugia kuku ambalo litaweza kutunza kuku ili wasiweze kupatwa na madhara mbalimbali kama vile; kuliwa/kujeruhiwa na wanyama wakali, kuchukuliwa na wezi nk. Lakini banda bora pia litawasaidia kuku kuhimili mabadiliko mbalimbali ya hali ya hewa yanayoweza kujitokeza.
Sehemu ambayo inafaa kwa ujenzi wa banda bora ni ile ambayo inaweza kufikika kwa urahisi, iwe na mwanga wa kutosha, isiwe na upepo mkali na isiyoruhusu maji kusimama au kuingia ndani.
Banda
ni vema likawa la ukuta/mbao/mabanzi.matete/mianzi imara ili lishikilie
paa vizuri lisianguke. Kuta hizi zaweza kujengwa kwa matofali ya
saruji/matope/kuchomwa/mabanzi/mbao nk. Katika kuezeka waweza kutumia
mabati/vigae/nyasi. Banda ni vema likawa kubwa kulingana na kiasi cha
kuku na umri walionao. Kitu cha kuzingatia ni kwamba banda liwe na hewa
ya kutosha.
Kuku
wanaofugwa ndani ni vema wakatengenezewa uzio mpana (angalau Mita 8x10)
ili wapate mahali wanapoweza kuota jua, kupumzikia/kupunga hewa na
kufanya mazoezi (wawekee kamba/bembea/ngazi ndani ya banda). Hakikisha
kuwa banda ni imara na hawatoki nje ya banda na kwenda mbali ili uweze
kuwawekea chakula cha kutosha na maji na hata wale wanaotaga/kuatamia
wapate chakula na kurudi haraka.
Banda
likiwa kubwa na bora litapunguza magonjwa kwani litakuwa na hewa ya
kutosha ambayo itasaidia kupunguza joto na unyevunyevu usio wa lazima
bandani mwako. Hii itasaidia uingizaji oksijeni ya kutosha na kupunguza
hewa chafu zenye madhara kwa kuku. Pia litasaidia namna ya kufanya usafi
kwa urahisi na kupunguza vumbi ambalo linaweza kusababisha kikohozi kwa
kuku wako. Ni vema banda lisipungue Mita 3 kwenda juu.
Mambo muhimu ndani ya Banda.
- Sakafu nzuri (iliyotengenezwa kwa saruji/udongo ili isituamishe maji. Isiwe na nyufa ili iweze kusafishwa kwa urahisi.
- Hakikisha kuwa banda linakuwa na Viota (vitagio) vizuri kwaajili ya kutagia. Viota viwe na urefu wa Sentimita 30 na upana sentimita 30 na kina sentimita 35. Sehemu ya mbele izibwe kwa sentimita 10 tu chini. Sehemu zote hizo zizibwe kwa ubao. Kama kuku wako ni wakubwa unaweza kuongeza upana, urefu na kina kiasi cha kutosha mfano, Upana na Urefu 35cm, kina 55cm nk. Hakikisha kiota/kitagio kinakuwa na giza kiasi maana kuku hupenda kutaga mahala pa giza kidogo/palipojificha. Giza litasaidia kuku asiweze kula mayai au asiweze kudonoana na kuku wengine. Kiota pia kinatakiwa kiwe mahali ambapo ni rahisi kwa kuku kuingia na kutoka, pia iwe ni rahisi kusafisa.
Ndani
ya kiota kuwekwe majani makavu/maranda ya mbao laini na kinyunyize dawa
ya unga ya kuzuia viroboto/utitiri kabla ya kuweka nyasi.
AIDHA, ni vizuri sana kuwawekea kuku wanaoatamia mayai wakati wa usiku maana ukimuwekea wakati wa mchana anaweza kuyaacha.
Kuku anayetarajiwa
kuatamia ni vema akachunguzwa kama anao utitiri/viroboto/chawa kwenye
manyoya yake. Wadudu hawa humkosesha raha kuku anayeatamia na wengi
huacha mayai na kukimbia/wasitulie kwenye viota vyao. Hali inapelekea
kuanguliwa kwa vifaranga wachache. Unaweza kumuona mtaalam wa mifugo kwa
ushauri zaidi.
- Banda liwe na vichanja maana kuku hupenda kulala juu ya vichanja maana nao ni ndege.
- Vyombo safi na vizuri kwaajili ya chakula na maji.
- Walazie majani makavu/maranda ya mbao/makapi ya mazao sakafuni kwa banda zima.
Mayai
huharibika kwa urahisi sana yasipo tayarishwa na kutunzwa vizuri kwa
uangalifu. Matayarisho huanzia bandani hadi ndani kwa kufanya yafuatayo;
- Hakikisha viota vyote ni safi wakati wote.
- Chakula kiwe ni cha kuimarisha gamba la yai na vyakula vingine.
- Vyombo vya kukusanyia mayai viewe safi na imara.
- Kusanya mayai mara2 hadi 3 kwa siku ili kuepuka mayai kuvunjwa/kuliwa/kuchafuka kwa mayai mengi na kupoa haraka.
- Ondoa mayai yaliyo na nyufa na maganda yasiyo imara.
- Safisha mayai mara baada ya kukusanya na kabla ya kuweka kwenye chombo cha kuhifadhia saa 12-24. Mayai yanaweza kuoshwa kwa maji ya uvuguvugu (nyuzijoto 35oc) na kusugua taratibu kwa mkono ili kuondoa uchafu (kama upo). Lakini unashauriwa kusugua kwa mkono bila maji ili kusafisha maana maji hupunguza ubora wa yai na maranyingi yai huharibika haraka.
- Weka katika vyombo visafi kwa kuelekeza sehemu ya yai iliyo pana iwe juu na sehemu nyembamba iwe chini, beba kwa uangalifu.
- Hifadhi mayai katika sehemu ya baridi nyuzijoto10 hadi 16 za sentigredi.
- Mayai yapangwe kwa daraja kwa kufuata ukubwa na rangi ili kuvutia wateja na kuongeza bei. Pia unaweza kuweka kwa kufuata muda unapoyaokota kutoka bandani. Weka lebo yenye tarehe ili usichanganye wakati wa kuwaatamishia kuku wako/kuuza.
Kuchagua mayai ya kuatamishia kuku kwaajili ya kuangua vifaranga.
Mayai
yanayofaa kwa kuatamiwa na kuanguliwa ni vema yawe na ukubwa wa
wastani, yasiwe na ufa/nyufa, yasiwe ya mviringo kama mpira, yasiwe na
uchafu wowote juu ya gamba lake, yasiwe yametengwa kwa zaidi ya wiki 1
(siku 7).
Kuna njia kuu mbili za ufugaji wa kuku.
- Ufugaji Huria
Aina
hii ya ufugaji, kuku huachiwa huru wajitafutie chakula na maji wao
wenyewe. Utaratibu huu hutumika zaidi kufugia kuku wa kienyeji ambapo
mfugaji hupata hasara na pengine hupata faida kidogo maana kuku hukosa
uangalizi na hawapewi chakula cha ziada.
Faida.
- Haina gharama kubwa za ufugaji.
- Kuku hupata mazoezi ya kutosha.
Hasara.
- Huharibu mazingira maana hula nafaka, mazao nk.
- Ni rahisi kuambukizwa na kusambaza magonjwa.
- Ni rahisi kuathiriwa na hali mbaya ya hewa, watu na wanyama wakali kama paka, vicheche, mwewe, kipanga, nyoka nk.
- Ni rahisi kutaga mayai porini/vichakani na hivyo mayai/kuku mwenyewe kupotea.
- Ukuaji wake ni hafifu/uliodhorota.
- Kuna uwezekano wa kuhamia nyumba nyingine/kwa jirani kwa urahisi.
- Ufugaji wa ndani ya Uzio/Banda.
Hufanyika
katika sehemu iliyozungushiwa uzio/ndani ya uzio maalum ambapo kunakuwa
kuna utaratibu wa kuku kupewa chakula na maji kwa urahisi. Ndani ya
uzio huwekwa banda zuri, bora na imara ambalo huruhusu kuku kuingia na
kutoka wanapopumzika/kulala/kutaga mayai. Ufugaji huu hutumika zaidi kwa
kuku wa kigeni na kuku chotara na hata wa kienyeji pia.
Faida.
- Gharama ya ufugaji wake ni kubwa.
- Faida yake ni kubwa hasa ukufuga kibiashara.
- Ni rahisi kuelewa kiwango cha utagaji na utotoaji wa kuku wako.
- Ni rahisi kufahamu kuku wazuri wa kuatamiashia mayai na kulea kwa faida ya haraka.
- Siyo rahisi kuku kuathiriwa na wezi/wanyama/vicheche/mwewe/hali mbaya ya hewa.
- Siyo rahisi kuambukizwa magonjwa mbalimbali kutoka nje.
- Ni rahisi kutibu na kujua maendeleo ya kuku wako kwa urahisi.
- Wanakuwa na usalama wa uhakika.
- Faida zake ni nyingi kuliko ufugaji huria.
Hasara
- Gharama za mwanzo za ujenzi wa banda, uzio na vifaa vya chakula na maji ni kubwa kiasi. Hivyo zinahitaji mtaji.
- Njia hii inahitaji eneo kubwa na huru.
- Ni rahisi kuambukizana ugonjwa kama itatokea.
- Ufugaji huu unahitaji utaalam na umakini wa kutosha
UCHAGUZI WA KUKU.
Chagua kuku wenye sifa zifuatazo;
- Wenye kukua haraka,
- Wenye uwezo wa kustahimili magonjwa,
- Wanaotaga mayai mengi,
- Wawe na uwezo wa kuatamia na kuangua vifaranga wengi na kuwalea (jike/mtetea).
Ni
vema sana kutumia majogoo chotara au majogoo wa kienyeji wale wakubwa,
warefu, wenye kucha fupi. Chagua wenye maumbile mazuri, uzito wa wastani
na wawe wenye rangi za kuvutia kisha uwachanganye na majike/mitetea
yenye umbo zuri, uzito mzuri na rangi nzuri ili kupata kuku chotara
wanaokua haraka na wenye uzito mzuri kwaajili ya biashara nk. Kama huna
kuku wenye sifa hizo basi ni bora sana ukanunua kutoka mahali pengine.
Wakati
wa kuatamia ni vema kuku mmoja apewe/awekewe mayai 12 hadi 15 kwenye
kiota chake mwenyewe na siyo kuwachanganya kama wakati wa kutaga maayai.
Kama wametotoa kuku 2 au zaidi kwa wakati mmoja ni vema aangaliwe kuku
mwenye uwezo wa kulea vifaranga ili aachiwe vifaranga vyote (kama
utashindwa kuwatengenezea boksi/kibanda cha vifaranga kama nilivyoshauri
hapo juu) na kuku wengine watengwe na vifaranga ili waanze kulishwa
vizuri na kuchanganywa na majogoo, hapa wataanza kutaga baada ya wiki 2
hivi.
MUHIMU: Ni vema sana kutofautisha makundi ya kuku kulingana na umri wao ili kupunguza kuku kudonoana/kuumizana.
- MAJI.
Maji
ni muhimu sana kwa kuku wawapo bandani. Wape maji ya kutosha kila
wakati unapoona yanapungua/kuisha ili waendelee kuyeyusha chakula
wanachokula Nna kupunguza joto mwilini. Kuku 1 anaweza kunywa hadi robo litaya
maji kwa siku. Kwa hiyo utawawekea kulingana na wingi wao. Pata chombo
kizuri ili uwaning’inizie juu kidogo kutoka usawa wa ardhi. Hii
itasaidia kupunguza uchafuzi wa maji na magonjwa yanayoenezwa kwa njia
ya maji.
ZINGATIA= hakikisha kuwa maji ni safi na salama.
- CHAKULA.
Ni
vema kutafuta vifaa vizuri kwaajili ya kuwawekea chakula. Tafuta vyombo
ambavyo utaweza kuning’iniza/tundika juu kidogo kutoka chini kulingana
na umri wa kuku. Hii itasadia sana kupunguza uwezekano wa kutosambaa kwa
magonjwa hasa yale yanayoenezwa kupitia viatu tunvyo vaa tunapoingia
bandani. Pia itasaidi sana kupunguza chakula kinacho mwagika chini
wakati kuku wanapokula.
Kwa
mfugaji yeyote wa kuku anapaswa kuelewa kuwa chakula cha kuku ni ghali.
Hivyo ni vema kufuata taratibu vizuri katika ulishaji na
kutengeneza/kununua vyombo ambavyo kuku hataweza kumwaga chakula.
Kumbuka kwamba kama vyombo siyo vizuri basi vitamwaga chakula kingi na
hivyo kukuletea hasara.
Ili
kuweza kupata mazao mazuri yenye faida, ni vema ununue chakula cha kuku
madukani au utengeneze wewe mwenyewe kama nitakavyoeleza hapa chini ili
uwape kuku wako chakula chenye viini lishe vyote muhimu kwa kuzingatia
umri wa kuku ulionao. Kwa vifaranga, unaweza kuwawekea chakula chini
kwenye magazeti/mifuniko ya ndoo/sahani. Baada ya siku 10 unaweza
kuwawekea kwenye chombo maalum.
Namna ya kuandaa chakula cha kuku.
Vyakula vya kuku vinapaswa kuwa na aina/viini lishe muhimu kama vile Protini, Wanga, madini na Vitamini.
Vyakula hivyo vimegawanyika kama ifuatavyo;
- Vyakula vya kujenga mwili ni; Jamii ya kunde,samaki, dagaa,mashudu ya ufuta/alizeti/pamba,
- Vyakula vya kulinda mwili ili usipatwe na maradhi ni; Mafuta ya samaki na majani mabichi kama vile; kabichi, mchicha,majani ya mpapai na nyasi mbichi.
- Vyakula vinavyojenga mwili/mifupa ni kama vile; Aina za madini, chokaa, chumvi na mifupa iliyosagwa.
- Vyakula vilivyotajwa vinaweza kumkuza vizuri kuku hadi uuzwaji/kuliwa kwake. Surghum Larrymeal huzuia kudonoana, huboresha kiini cha yai na kuongeza mayai. Changanya kg 1 kwa kg 50 za pumba.
Ukosefu
wa madini kama fosforasi na kalsiam husababisha matege, vidole
kukunjamana, kufyatuka kwa misuli ya magoti, kuwa kilema na kupofuka
macho kwa kuku.
Mfugaji
wa kuku anaweza kununua vyakula hivi kwenye maduka ya pembejeo za
kilimo/mifugo. Na kama huwezi unaweza kujitengenezea wewe mwenyewe kwa
kukusanya mahitaji muhimu ya viinilishe kama ifuatavyo hapa chini;
Aina ya chakula | Kiwango cha uchanganyaji (%) | ||
Vyakula | Vifaranga (Kgs) | Kuku wa Nyama (Kgs) | Kuku wa Mayai (Kgs) |
Mahindi | 70 | 70 | 70 |
Ulezi | 20 | 40 | 40 |
Mtama | 20 | 30 | 30 |
Mpunga | 40 | 70 | 70 |
Ngano | 5 | 40 | 40 |
Pumba za Mahindi | 10 | 20 | 20 |
Pumba za Mpunga | 10 | 20 | 20 |
Pumba za Matama | 10 | 20 | 20 |
Pumba za Ngano | 5 | 15 | 15 |
Mashudu ya Nazi | 10 | 30 | 40 |
Mashudu ya Pamba | 5 | 10 | 10 |
Mashudu ya Alizeti | 10 | 20 | 20 |
Mashudu ya Ufuta | 10 | 10 | 5 |
Damu iliyokaushwa | 5 | 5 | 5 |
Mifupa iliyosagwa | 5 | 5 | 7.5 |
Dagaa | 10 | 5 | 5 |
Lucina | 5 | 5 | 5 |
Chokaa | 5 | 5 | 5 |
Chumvi | 0.5 | 0.5 | 0.5 |
Soya | 10 | 20 | 20 |
Sorghum Larry Meal | 1 | 1 | 1 |
NB. Kabla ya kufanya kazi hii unaweza ukamuona mtaalam wa mifugo kwa ushauri zaidi kama utaona ni muhimu.
Mfano wa namna ya kuandaa kilo 100 za chakula cha kuku.
- Mfano wa chakula cha vifaranga kuanzia umri wa siku 1-wiki 4.
VYAKULA | KIASI(Kilogram) KG |
Mahindi | 30kg |
Pumba za Mahindi | 20kg |
Soya | 18kg |
Mashudu ya Alizeti | 20kg |
Dagaa | 5kg |
Mifupa iliyosagwa | 4kg |
Chumvi | 0.5kg |
Vitamini | 2.0kg |
Jumla 100 |
- Mfano wa chakula cha kukuzia kuanzia Wiki 4-8
VYAKULA | KIASI(Kg) |
Mahindi | 45kg |
Pumba za Mahindi | 20kg |
Mashudu ya Pamba | 5.0kg |
Soya | 20kg |
Dagaa | 2.5kg |
Mifupa iliyosagwa | 5.0kg |
Chumvi | 0.5kg |
Vitamini/Damu kavu | 2.0kg |
Jumla 100 |
Kuku huweza kushambuliwa na magonjwa mengi ambayo mara nyingi husababisha hasara kubwa kwa mfugaji. Hasara hizo ni kama vile; gharama za matibabu, upungufu wa mayai, kudumaa kwa kuku, na vifo.
Magonjwa ya kuku yamekuwa ni tishio na hukatisha tamaa sana watu wanaofuga kuku. Magonjwa mengi husababishwa na Bakteria, Virusi, Vimelea, Minyoo, Viroboto, Chawa, Utitiri, Lishe duni au Uchafu. Lakini
sauala hili limegundulika kuwa mara nyingi makosa ni ya wafugaji
wenyewe kwani maranyingi hupuuzia suala la umuhimu wa kuwaona wataalam
wa mifugo (ndege) na baadhi wanapobahatika kuwaona wataalam, basi
hupuuzia ushauri wa wataalam hao.
Baadhi
ya magonjwa hayo na njia rahisi ya kuyatibu ni kama ifuatavyo
(nimejitahidi kutafsiri kidogo,lakini maneno mengine ni ya kiingereza
ambayo sikupata tafsiri yake kwa urahisi);
MAGONJWA YA NDEGE WANAOFUGWA MAJUMBANI
(HASA KUKU)
JINA LA ASILI | DALILI | KISABABISHO (PRESUMPTIVE DIAGNOSIS) | DALILI KUU (CLINICAL SIGNS) | MATIBABU RAHISI LAKINI MUHIMU NA HARAKA TENA KWA GHARAMA NAFUU |
Kideri/ Mdondo (Newcastle Disease) | Kusinzia, kuhara, kushusha mabawa chini, kukosa hamu ya kula nk | Newcastle Virus | Kuku kuharisha kinyesi cha kijani/cheupe km chokaa na njano, kukohoa, kuhema kwa shida, kutokwa na mate mdomoni,kizunguzungu, kishiwa na maji, kukosa hamu ya kula,kushusha mabawa chini,kuku kufa hadi 90%. |
|
Ndui (Fowl Pox) | Vipele kwenye upanga (Nodules) na sehemu zisizo na manyoya. | Fowl pox | Vipele kwenye upanga,masikio.miguu na sehemu zisizo na manyoya.Kuku hufa hasa wale wadogo. |
|
Mafua ya kuku/ Kuvimba macho | Swollen eyes/ Flu | Bakteria | Kuvimba uso na macho,kamasi hutiririka kutoka puani na mdomoni,hukohoa,huhema kwa shida na kukoroma, utando mweupe/njano kwenye macho),upofu,nk | Boresha Usafi wa banda na mazingira yake, kuku wagonjwa watengwe na ikibidi wachinjwe. Muone mtaalam wa mifugo ili upate chanjo. |
Ugonjwa unaoshambulia mfumo wa hewa. | Chronic Respiratory infection. | Infections bronchitis laringotracheitis/Chicken Influenza (Bakteria) | Kuku hupata Mafua, kushindwa kupumua,hutokwa na makamasi,vifaranga hudumaa,utagaji hupungua na viungo vya mifupa huvimba. | Boresha usafi, hakikisha kuna hewa ya kutosha. Muone mtaalam akupe antibayotiki huponya/kwa ushauri zaidiTenganisha kuku wenye ugonjwa. |
Gumboro/Kuhara chokaa | Whitish diarrhoea | Fowl typhoid | Vifaranga kuharisha kinyesi cheupe, kupungua uzito,hushindwa kuhema,manyoya husimama,hutetemeka na hatimaye hufa. | Chanja vifaranga wakiwa na umri wa siku 1. Zingatia usafi wa banda, vyombo vya maji na chakula. Tumia mkaa. Hakuna tiba ya kitaalam |
Viroboto/ Utitiri/ | Fleas/mites | Ectoparasites | Fleas around the eyes, Restlessness (Kutulia kwa muda mrefu bila kuchangamka) | Tumia kuweka majivu bandani. Kitaalam tumia dawa yenye unga kama poda. |
Papasi | Soft ticks | Soft ticks | Sores on skin(Vidonda kwenye ngozi), Paralysis(ku, Anaemia | Tumia kuweka majivu bandani. Kitaalam tumia dawa yenye unga kama poda. |
kunyonyoka manyoya | Minyoo/bacteria | Kunyonyoka manyoya na kubaki mtupu. Shingo kurudi nyuma, kushindwa kula vizuri. | Tumia kinysi cha n’ombe. Kitaalam tumia Vitamin B12 na Egg Plus Fomula. | |
Kuhara choo cheupe | White Bacillary Diarrhoe | Zaidi ni kwa vifaranga kabla ya wiki 4 kuhara mharo mweupe. | Tumia mkaa, Alovera. Kitaalam tumia OTC+ | |
Homa ya matumbo | Bloody diarrhea/ Typhoid | Coccidiosis | Ugonjwa huu huambukizwa kupitia maji/mayai/kinyesi/kudonoana na mazingira machafu. Kuku huharisha mharo wa kijani, vilemba na upanga hupauka kutokana na upungufu wa damu,manyoya kusimama. | Tumia mkaa, Alovera. Vitunguu swaumu robo kilo ikitolewa maganda,ikatwangwa na kuchanganywa na maji lita 1,chuja na kuwapa maji yake kwa wiki 1. Ondoa kuku wenye ugonjwa na usitumie mayai yenye ugonjwa kuanguliwa vifaranga. Kitaalam tumia Furazolidone. Muone mtaalam |
Kuvimba miguu | Swollen legs | Scaly legs | Scales on legs(mikato miguuni), lameness. | Tumia Alovera Muone mtaalam |
Kipindupindu cha kuku | Fowl Cholera | Bacteria | Mharo wa njano, husinzia na kulegea,hulala kichwa kikining’inia kwenye mabawa,manyoya husimama,hushindwa kuhema na hatimaye hufa. | Imarisha usafi wa banda,vyombo na mazingira yake. Kitaalam unaweza kutumia dawa aina ya Salfa/muone daktari. |
Mayai kuvunjika tumboni | Broken eggs in abdomen | Egg peritonitis | Sleepy, on PM broken eggs with foul smell | Muone mtaalam kwa ushauri. |
Kwa kutumia dawa za asili nilizosema hapo juu;
- Pilipili kichaa 50, twanga, changanya na majivu kikombe cha chai 1, weka maji Lita 1 wape kuku.
- Katani/alovera. Ipondeponde, iloweke kwenye maji usiku kucha, wape wanywe.
- Mkaa. Kama kuku wako wanaharisha,Chukua kiasi cha mkaa, kitwange, changanya kwenye chakula, wape, hawataharisha tena. Mama E.G.White katika kitabu chake cha Uponyaji wa Mungu Uk.64 ameeleza juu ya Tiba ya Mkaa. Jaribu uone mafanikio yake kwa kuku anyeharisha kawaida na siyo kideri.
- Kinyesi cha Ng’ombe. Kausha kinyesi cha ng’ombe, kisage na kisha changanya na chakula cha kuku. Hii inasaidia sana kwa kuku wanaonyonyoka manyoya.
MINYOO.
Hawa
ni wadudu wanaoleta madhara kwa kuku na wanyama wengine pia. Kuku
hupata minyoo kwa kula vyakula vyenye wadudu/vimelea vya wadudu hao.
Dalili. Kuku Hudumaa, manyoya huwa hafifu, hupungua damu na uzito, utagaji wa mayai hupungua, minyoo huweza kuonekana kwenye kinyesi.
Namna ya kuzuia minyoo.
- Safisha banda mara kwa mara (ukiweza tumia dawa za kuua wadudu)
- Badilisha matandazo mara kwa mara.
- Safisha vyombo vya chakula na maji mara 2/3 kwa siku.
- Tenganisha kuku wakubwa na wadogo.
- Wape kuku dawa za kuzuia minyoo kila baada ya miezi 3.
- Muone mtaalam kwa ushauri zaidi.
MAGONJWA YANAYOWEZA KUSABABISHWA NA UPUNGUFU WA CHAKULA/VIINI LISHE.
Iwapo kuku watapewa chakula chenye viini lishe kidogo/kisicho na viini lishe muhimu kama vile; Protini, Wanga, Madini na Vitamini wanaweza kupata madhara yafuatayo;
- Kudumaa,
- Kupungua uzito,
- Kupungukiwa na damu,
- Mifupa kupinda/kuvimba/kutokuwa imara,
- Utagaji wa mayai hupungua na uangaji wake pia huwa hafifu,
- Ganda la yai huwa laini,
- Manyoya huwa machache na laini,
- Kujikunja kwa shingo/miguu na vidole,
- Kuwa na majimengi mazito chini ya ngozi ya kifuani,
- Kupata magonjwa mara kwa mara,
- Hali hii inaweza kusababisha Kuku kufa.
Namna ya kuzuia.
- Kuku wapewe chakula chenye mchanganyiko wa viinilishe vyote muhimu kama vile Vitamini, madini na Chokaa kufuatana na umri/aina na mahitaji yake.
- Wapewe majani mabichi kama mchicha, kabichi na majani ya mapapai.
- Wapewe mchanganyiko wa vitamin na madini kama chokaa na chumvi kwa kiwango maalum maana ikizidi pia yaweza kuathiri kuku.
MUHIMU.
Ili
liziua magonjwa ya kuku na kupata faida kubwa kwa kufuga kuku, ni
muhimu sana mtu anayehudumia kuku bandani aweze kutambua haraka dalili
za magonjwa ya kuku kama nilivyoeleza hapo juu ikiwa ni pamoja na
kuzingatia usafi wa banda. Ni lazima ajue tabia ya kuku ya kila siku.
Kuku mgonjwa unaweza kumtambua kwa kuangalia yafuatayo;
- Tabia ya kuku.
- Kinyesi cha kuku (mabadiliko ya kinyesi).
- Ulaji wa chakula na unywaji wa maji kama umepungua.
- Utagaji wa mayai na uimara wa mayai kama vimepungua.
- Kuku kutochangamka.
- Vifo ni dalili ya mwisho.
Kama
utaona kuna kuku mgonjwa bandani basi mtenge na wenzie kama
unavyowafanyia vifaranga. Ili uweze kuwahudumia peke yao. Wengine ambao
hawajaonesha dalili wapewe dawa ya kinga haraka iwezekanavyo kupitia
ushauri wa mtaalam wa mifugo aliye karibu.
Chanjo
na matibabu yoyote yafuate ushauri wa mtaalam/mtengenezaji wa dawa
husika bila kupuuzia ili upate mafanikio. Hii itakuwezesha
kupunguza/kuponya magonjwa na kupunguza gharama za matibabu na vifo.
Hakikisha kuwa chanjo/tiba zinatoka kwa mtaalam anayejua kutunza
chanjo/dawa kwenye ubaridi unaotakiwa kulingana na maagizo ya
mtengenezaji.
ANGALIZO
Mambo yafuatayo yanaweza kusababisha magonjwa au kupunguza uzalishaji hivyo kuleta hasara zisizo za lazima kwa mfugaji.;
- Kufuga kuku wengi kwenye eneo dogo.
- Chumba/banda lisilo na hewa na mwanga wa kutosha.
- Banda kuwa chafu.
- Vyombo vichache/visivyotesheleza kwaajili ya chakula na maji.
- Vyombo vichafu vya maji na chakula.
- Chakula kisicho na viini lishe vya kutosha/kichache.
- Kubadili ladha ya chakula.
- Kuchelewa kudhibiti magonjwa ya kuku.
- Kuchanja/kutibu kuku bila utaratibu/ushauri wa kitaalam.
- Kutishia kuku wakati wa kuingia bandani/kuwashika/kuwasumbuasumbua.
- Mabadiliko ya hali ya hewa.
- Kufuga kiholela bila kuwachambua.
MWISHO
- Chagua njia bora na rahisi inayokufaa kulingana na eneo ulilopo na mahitaji yako pia. Angalia njia itakayokupa faida kwa gharama ndogo.
- Chagua kuku wenye uwezo wa kukua haraka, wanaostahimili magonjwa, wanaotaga mayai mengi, wanaoweza kuangua vifaranga wengi na kuwalea.
- Chagua jogoo aliye na uzito mzuri na mwenye kucha fupi.
- Uwiano wa jogoo kwa majike iwe ni jogoo 1 kwa majike/mitetea 10.
- Kuku anayetazamiwa kuatamia mayai anatakiwa asiwe na chawa/viroboto/utitiri.
- Kuku ambaye hakidhi sifa za kuwa kuku bora anayefaa kuwa kwenye kundi inafaa aondolewe ili asilishwe kwa hasara awapo bandani.
Waafrika
tulio wengi hatuna utamaduni wa kutunza kumbukumbu. Ni vizuri basi
uanze kutunza kumbukumbu za mwenendo wa kazi zako za ufugaji wa kuku.
Hii itakurahishia sana kujua faida, hasara na hata kujua namna bora ya
kuboresha ufugaji wako. Kwa mfano;
- Kumbukumbu za uzalishaji mayai zitakuwezesha kujua kiasi cha mayai yanayotagwa kwa siku. Idadi ikiwa chini ya 60% utagaji huo siyo mzuri hivyo utatafuta sababu ya tatizo nk. Utagaji unatakiwa uwe 70% hadi 95%.
- Kumbukumbu ya vifo itakusaidia kujua hatari itakayokujia. Mfano vifo vikizidi 1% inaashiria tatizo la ugonjwa. Hivyo uchunguzi ni lazima ufanyike ili kutatua tatizo.
- Kumbukumbu za mapato na matumizi pia zitakusaidia kujua faida na hasara nk. Hapa utajua ni ghara kiasi gani ulitumia kufuga na faida kiasi gani umepata baada ya mauzo ya mayai/kuku husika. .............................................................................................
0 comments:
Post a Comment