script>" " ".

Get our Android App in Playstore DOWNLOAD HERE!

X





                   

MAFUNZO KWA WAFUGAJI


MADA 1
UTANGULIZI
Ufugaji wa ng’ombe wa maziwa ni shughuli yenye tija kubwa na yenye kuongeza kipato kwa jamii na lishe kwani maziwa yana viinilishe muhimu vinavyohitajika mwilini. Ng’ombe wa maziwa ni kama kiwanda ambacho hubadilisha chakula (majani) kuwa maziwa pamoja na maziwa pia kinyesi cha ng’ombe hutumika kama mbolea na chanzo cha nishati (biogas).
Hata hivyo ili kupata faida kubwa katika ufugaji wa ng’ombe wa maziwa ni muhimu mfugaji azingantie kanuni za ufugaji bora.

MAMBO YA KUZINGATIA
1.    Uchaguzi wa ng’ombe wa maziwa
2.    Banda la kufugia ng’ombe wa maziwa
3.    Lishe ya ng’ombe wa maziwa
4.    Uthibiti wa magonjwa
5.    Utunzaji wa kumbukumbu za ufugaji.

1.0. UCHAGUZI WA NG’OMBE WA MAZIWA
Wakati wa uchaguzi wa aina ya ng’ombe wa maziwa atakayekufaa  kwa ufugaji ni vyema kuzingatia vigezo vifuatavyo.
1.    Sifa za uzalishaji wa maziwa na uvumilivu wa magonjwa na hali ya hewa
2.    Uwezo wa kumlisha na kumpatia huduma nyingine muhimu kwa ajili ya matunzo yake
3.    Uhakika wa upaikanaji wa aina hiyo ya ng’ombe
4.    Uwezo wa kifedha (mtaji).

 2. 0. BANDA LA NG’OMBE WA MAZIWA
Banda la ng’ombe ni vyema liwe bora kwani hurahisisha kazi ya ufugaji na kuwezesha mifugo kuishi mahali pazuri na safi hivyo kuwezesha ng’ombe kuwa na afya nzuri na kupelekea upatikanaji wa maziwa mengi  ambayo ni safi na salama kwa matumizi ya binadamu.

2.1. SABABU YA UJENZI WA BANDA BORA.
1.    Kupunguza uwezekano wa maambukizo ya magonjwa kama ugonjwa wa kiwele n.k
2.    Huwezesha kutoa huduma rahisi kwa ng’ombe wako
3.    Huzuia athari za jua kali na mvua
4.    Uhakika wa mahali pazuri pa kulala, chakula safi na maji ya kutosha wakati wote
5.    Kumlinda ng’ombe na wezi pamoja na kutoshambuliwa na wanyama wakali.

Chakula anachopatiwa ng’ombe ni vyema kiwe na uwezo wa kuupatia mwili viinilishe vinavyohitajika kwa ajili ya ukuaji, nguvu na kinga.Viinilishe hivi ni Wanga, Protini, Madini, Vitamini na Madini. Mahitaji ya viinilishe mwilini hutofautiana kulingana na hatua mbalimbali za ukuaji,wakati wa mimba na wakati wa utoaji maziwa na hivyo kukosekana kwa  viinilishe hivyo katika vipindi hivyo huweza kusababisha ng’ombe kudumaa, motto kufia tumboni au kufa baada ya kuzaliwa na iwapo ataishi atakuwa mdhaifu na utoaji wa maziwa kidogo na kama ni dume kushindwa au kupunguza uwezo wa kupanda.
Mara nyingi kipindi cha ukame malisho huwa haba, kwa hiyo ni vizuri kuhifadhi malisho yanapokuwa mengi ili yaweze kulishwa kipindi cha uhaba wa malisho.

3.1. MAKISIO YA MAHITAJI YA MALISHO KWA NG’OMBE KWA SIKU
Kiasi cha malisho kinachotakiwa kwa ng’ombe kwa siku hutegemea ukubwa wa ng’ombe (3% ya uzito wake kwa majani makavu), hali ya hewa, kisi cha maji kilichoko kwenye malisho, kiasi cha vyakula vya ziada anachopata kwa siku, hali ya ng’ombe (ana mimba/hana, anakamuliwa/hakamuliwi) na kiwango cha uzalishaji maziwa.


Makundi ya ng’ombe (umri)
Kiasi cha Malisho
vyakula vya  ziada

Mvua (kilo)
Kiangazi (kilo)

Ng’ombe wakubwa
80-120
65-80
5-8
Ng’ombe wanaokua
50-80
40-65
3-4
Ng’ombe wadogo
30-50
25-40
1-2

Hata hivyo ulishaji wa vyakula vya ziada inashauriwa vitumike pale tu ghrarama yake inapokuwa ndogo kulinganisha na thamani ya maziwa yanayotarajiwa kuongezeka.
Kipimo cha kulisha vyakula vya ziada kwa ng’ombe anayekamuliwa.
Kama chakula ni mchanganyiko maalumu (Dairy meal) kwa kila lita 2-3 za maziwa anayotoa ng’ombe apewe kilo moja ya chakula hicho.Iwapo pumba itatumika  ng’ombe alishwe kilo moja na nusu  za pumba kwa kila lita 2-3 za maziwa anazotoa.
Angalizo; Iwapo ng’ombe tayari anatoa maziwa katika uwezo wake wote ni hasara kiuchumi kumlisha vyakula vya ziada kwani vitaongeza gharama za uzalishaji na kumfanya ng’ombe anenepe kupita kiasi na kusababisha matatizo ya kushika mimba na kusababisha viwele kuwa na mafuta mengi jambo ambalo linaweza kupunguza uwezo wa kutengeneza maziwa.

4.0. UDHIBITI WA MAGONJWA
Ili kulinda Afya ng’ombe, Watumiaji wa maziwa na kuongeza kiwango cha maziwa kinachozalishwa ni vyema kumkinga ng’ombe na magonjwa ya aina mbalimbali. Uzuiaji wa magonjwa hupunguza gharama za matibabu, hasara zinazotokana na kushuka kwa uzalishaji pamoja na kuongezeka kwa vifo vya ngo’mbe vinavyotokana na magonjwa. Mfugaji anashauriwa kufuata ushauri wa kitaalamu kutoka madaktari wa mifugo katika kuzuia magonjwa na utoaji wa chanjo kwa magonjwa mbalimbali.

5.0.      UTUNZAJI KUMBUKUMBU
Utunzaji kumbukumbu ni muhimu kwani humwezesha mfugaji kuelewa kiasi cha faida anayopata kutokana na shughuli anayofanya pamoja na maendeleo ya ng’ombe wake;

5.1.      FAIDA ZA  KUWEKA KUMBUKUMBU
1.    Kuwa na taarifa kamili za sifa za kila ngo’mbe na ukoo zao
2.    Kupanga upandishaji kwa wakati
3.    Uzuiaji magonjwa
4.    Kujua uzalishaji maziwa
5.    Kujua mapato na matumizi
6.    Kupanga mipango ya kuendeleza mradi
5.2.      AINA ZA KUMBUKUMBU.
1.    Kumbukumbu ya wataalam na ushauri waliotoa
2.    Kumbukumbu ya  kinga na Afya ya ng’ombe
3.    Kumbukumbu ya  uzalishaji,uuzaji na utumiaji maziwa
4.    Kumbukumbu ya  uzalishaji-upandishaji,uingiaji kwenye joto na kuzaa
5.    Kumbukumbu ya mapato na matumizi ya mradi

MADA 2.
1.0.      UZALISHAJI NA USAMBAZAJI WA MAZIWA
Maziwa yanayokamuliwa kutoka kwenye ng’ombe mwenye afya yanakuwa na bakteria wachache sana. Uchafu unaingiza bakteria wanaosababisha maziwa kuharibika haraka. Ili kuhakikisha maziwa yanaendelea kuwa freshi kwa muda mrefu zaidi unahitaji usafi wa ukamuaji na utunzaji wa maziwa.

1.1. Mambo muhimu yanayochangia ubora wa maziwa
1.1.1. Ulishaji
Mnyama aliyelishwa vizuri na kupata maji ya kutosha huzalisha maziwa mengi yenye virutubisho vya kutosha.

1.1.2. Afya ya Ng’ombe
Ng’ombe asiye na afya hali chakula vizuri na huzalisha maziwa kidogo na yasiyo na ubora unaotakiwa. Wakati wote ng’ombe anatakiwa kuwa msafi na mwenye afya kwa sababu wanyama wagonjwa hueneza magonjwa kama vile kifua kikuu na ugonjwa wa kutupa mimba pamoja na homa za vipindi kwa watuamiaji wa maziwa. Ukihisi kuwa ng’ombe ni mgonjwa, wasiliana na mhudumu wa afya ya mifugo mara moja. Usiuze wala usinywe maziwa yaliyokamuliwa kutoka kwa ng’ombe aliyetibibiwa kwa dawa ya kiuavijasumu (antibiotics) hadi muda uliopendekezwa utakapokwisha

Kumbuka kuwa udhibiti wa ubora wa maziwa huanzia kwa mfugaji. Kwa kufanya hivyo, utapunguza kuwepo kwa bakteria wanaoharibu maziwa na kusababisha magonjwa. Ili kuhakikisha ubora na kulinda afya ya watumiaji huna budi kuzingatia utaratibu mzuri wa ukamuaji kama ifuatavyo:
  1. Hakikisha ng’ombe ni wenye afya na wasafi. Mifugo yenye maradhi inaweza  kueneza magonjwa kwa binadamu kupitia maziwa.
  2. Mazingira ya kukamulia yawe safi, yasiwe na vumbi wala matope. Taka na samadi katika eneo la kukamulia husababisha kuwepo kwa panya, mende na nzi ambao huingiza uchafu na bakteria kwenye maziwa.
  3. Usikamue maziwa ikiwa unaumwa magonjwa ya kuambukiza kama kuhara au homa ya matumbo hadi utakapotibiwa na kupona.
  4. Mkamuaji hatakiwi kuwa na kucha ndefu, kupiga chafya, kutema mate ovyo au kukohoa na kuvuta sigara.
  5. Usiyachanganye dang'a (maziwa yanayokamuliwa siku saba za mwanzo baada ya ng’ombe kuzaa) na maziwa ya kawaida.
  6. Nawa mikono kwa kutumia sabuni na maji safi kabla ya kukamua.
  7. Osha kiwele kwa kutumia kitambaa safi na maji ya uvuguvugu.
  8. Kausha kiwele kwa kutumia kitambaa kikavu na safi.
  9. Kabla ya kuanza kukamua paka mafuta maalum kwenye chuchu ili kuleta ulaini na kuepusha michubuko wakati wa ukamuaji.
  10. Kamulia kidogo kwenye kikombe maalumu kwanza, chunguza ugonjwa wa kuvimba kiwele kisha mwaga maziwa hayo mbali na eneo la kukamulia hata kama yakionekana salama kwa sababu maziwa ya mwanzo huweza kua na bacteria wengi zaidi.
  11. Tumia vyombo safi na vikavu vya kukamulia (aluminiamu au chuma kisichoshika kutu).
  12. Ng’ombe mwenye ugonjwa wa kiwele wakamuliwe mwisho na maziwa yao yamwagwe katika shimo na kufunikwa.
  13. Maziwa ya ng’ombe aliyetibiwa na vijiuasumu yasiuzwe wala kutumika baada ya matibabu mpaka pale itakavyoshauriwa na mtaalamu wa mifugo.
  14. Mara baada ya kukamua chovya chuchu katika dawa maalum (kemikali inayozuia kukua kwa bacteria).
  15. Baada ya kukamua chuja maziwa kwa kutumia chujio au kitambaa maalumu ili kuondoa uchafu
  16. Funika maziwa ili uchafu isiingie na hifadhi sehemu safi yenye ubaridi.

2.0. USAMBAZAJI BORA WA MAZIWA
Maziwa ni zao ambalo ni rahisi kuharibika endapo hayatatunzwa vizuri, na kusafirishwa vizuri na haraka ili yafike kiwandani yakiwa salama tayari kwa kusindikwa. Utunzaji wa maziwa unagusa kwenye usafi wa vyombo na joto la kuhifadhia maziwa. Bacteria wengi wanazaliana katika joto lililo kati ya nyuzi joto 250C-400C. Kuwakabili bacteria wasizaliane haraka ni lazima tuyahifadhi maziwa kwa joto la chini.

3.0. VYOMBO NA NAMNA YA UTUNZAJI WA MAZIWA
Vyombo vya aluminiamu na chuma kisichopata kutu ndivyo hutumika katika kushughulikia maziwa vikiwa safi vilivyooshwa vizuri.
Mahali pa kuhifadhia maziwa pawe safi pasipo kuwa na wadudu, penye hewa na mwanga wa kutosha, hapana vumbi wala mionzi ya jua na mvua haingii.
Maziwa yasihifadhiwe chumba kimoja na mazao ya kilimo kama kabichi, vitunguu, pumba n.k pia yasihifadhiwe mahali penye kemikali kama rangi, mafuta ya taa petroli, viwatilifu n.k
Safirisha maziwa haraka sana iwezekanavyo. ucheleweshaji wa kuyasafirisha utasababisha yaanze kuharibika. Maziwa yanauwezo wa kujitunza kwa masaa matatu tu baada ya kukamuliwa. Mfugaji ahakikishe maziwa yanafika kiwandani au kituo cha kukusanyia maziwa ndani ya masaa matatu.
  
4.0. NJIA MBALIMBALI ZA KUPOZA MAZIWA
Maziwa yanapo toka kukamuliwa, yanakuwa na joto la digrii 350C-370C. Kama hayakupozwa haraka na kusafirishwa kiwandani yana hatari ya kuharibika baada ya masaa matatu, kwani bacteria ndani ya maziwa wanapenda joto hilo kuzaliana.
Endapo kiwanda kipo mbali na alipo mfugaji ,au kwa maziwa ya jioni, ni vizuri mfugaji ayapoze maziwa kwa joto la chini kwa kwa kutumia njia zifuatazo ili kuyatunza mpaka yatakapo yasafirisha.
  1. Jokofu- Hii ni njia nyepesi ya kuhifadhi maziwa kwa mfugaji mdogo. Majokofu yanapatikana kwa wingi madukani, ni vizuri mfugaji anunuwe jokovu (kwa sehemu zenye umeme) ili kuhifadhi maziwa katika nyuzi joto 4-5oC mpaka atakapo yapeleka katika kituo cha kupoozea/kukusanyia au kiwandani.
  2. Kupoza kwa hewa-kwa maeneo yenye hewa baridi (chini ya digrii 100C hasa wakati wa usiku, Mikoa kama Njombe Mbeya, Arusha, Morogoro(mgeta) n.k. maziwa yanaweza kupozwa kwa kuwekwa sehemu ya wazi yenye baridi na kuyafanya yapoe vizuri, au unaweza kuloweka blanketi au gunia la maji na kulizungushia kwenye chombo chako cha maziwa. Hii itasaidia sana kushusha joto wakati yakiwa yanapata upepo.
  3. Kupoza kwa maji- kwa maeneo hayo hayo yenye baridi maji ya mito/bomba yenye baridi chini ya digrii 150C yaweza kutumika. 
  4. Ice bank- Hili ni tanki la wazi lililo fungwa vifaa vya kutengeneza barafu kwenye mabomba yanayo pita kwenye maji ya tanki na kufanya maji yawe baridi sana. Ice bank ni nzuri sana hasa kwa wenye viwanda vidogo.
  5. Ni vizuri maziwa yanapotoka kukamuliwa yapozwe na maji baridi kushusha nyuzi joto 37OC mpaka yawe baridi nyuzi joto 25oC kushuka chini, ili kurahisisha upozaji wa baadae wa jokofu au mashine nyingine za kupozea maziwa, ikiwa maziwa hayo yatasafirishwa baadae, au siku inayofuata.

Ili kuhakikisha ubora wa maziwa unatunzwa wakati wa kusafirishwa, mambo yafuatayo yazingatiwe.
1. Wahudumu wote wanaosafirisha maziwa wawe wasafi kuanzia kwenye mavazi, afya zao, wamekata kucha, punguza ndevu, nywele n.k
2. Vitumike vyombo maalumu vya metali.
3. Hakikisha vyombo hivyo ni visafi wakati wote.
4. Weka maziwa mbali na mionzi ya jua, vumbi na mvua na epuka kuhifadhi maziwa muda mwingi kwenye joto kali.
5. Maziwa yasafirishwe kiwandani ndani ya masaa matatu.
6. Zuia mtikisiko mkubwa wa maziwa kwa kuweka ujazo kulingana na uwezo wa chombo unachosafirishia, kutojaza maziwa inaweza kufanya maziwa kutengana na mafuta au kuleta povu na kusababisha maziwa yaharibike upesi.
7. Usibebe abiria wala wanyama kwenye gari la maziwa.

Tembelea hapa

0 comments:

 
Top